Madudu hayo, yanatajwa kuwa pengine ni makubwa kuliko hata yale 
yaliyoifanya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira,
 ishauri Kamati hiyo ivunjwe kutokana na tuhuma za rushwa miongoni mwa 
wajumbe.
Wajumbe kadhaa wametumia mwanya wa kuugua kwa Mwenyekiti
 wa Kamati, Bakari Mbano, kufanya mchezo huo. Kamati hiyo iliketi kwa 
siku mbili - Novemba 16 na 17, mwaka huu jijini Dar es Salaam - na 
kutengua baadhi ya uamuzi wake wa awali wa ugawaji vitalu, na kwa mara 
ya kwanza, kundi la matajiri wa kigeni wenye fedha limeweza kupendekezwa
 kupewa vitalu vinono ambavyo viliambuliwa na kampuni chache za wazawa.
Habari
 za uhakika zinaonyesha kuwa kampuni zaidi ya 10 zilizopewa vitalu 
awali, zimenyang’anywa; kwa kile kilichoelezwa kuwa ni utekelezaji wa 
maagizo ya Bunge ya kutaka kampuni zisizo na sifa, lakini zikapewa 
vitalu, zinyang’anywe.
Kwa kutumia mwanya huo, Kamati ya Ugawaji 
Vitalu imerejesha baadhi ya vitalu vilivyopendekezwa, lakini ikaenda 
mbali zaidi na kuwanyang’anya masikini wazalendo ambao walipewa vitalu 
hivyo baada ya kutimiza matakwa ya kisheria yaliyosimamiwa kwa ukaguzi 
wa kila kampuni.
Madai ya uamuzi wa kuwanyang’anya wazawa vitalu,
 yamefanywa kwa misingi ya rushwa na yanatokana na ukweli kwamba 
wanachama wa TAHOA (Chama cha Wamiliki wa Kampuni za Uwindaji wa 
Kitalii), ambao wengi ni wageni, hawakuguswa kabisa.
Kwa namna 
inayoibua harufu ya rushwa, vitalu hivyo vimekabidhiwa kwa kampuni 
nyingine, tena za wageni, bila kufuata utaratibu wa kuvitangaza, hata 
kama kweli walionyang’anywa hawakuwa na sifa. Kisheria, Serikali 
inapotwaa vitalu inapaswa kuvitangaza ili wanaovitaka waweze kuomba.
Uamuzi
 wa Kamati hiyo ulifanywa chini ya uenyekiti wa muda wa Jaji mstaafu, 
Steven Ihema, kutokana na Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri wa Ugawaji 
Vitalu, Bakari Mbano, kuugua.
Wazawa kupokwa vitalu hivyo ni 
kutimia kwa kauli za majigambo za wageni hao walizoanza kuzitoa Desemba,
 mwaka jana, ukiwa ni muda mfupi baada ya kutangazwa kwa matokeo ya 
ugawaji vitalu.
Desemba 12, Waziri wa wakati huo, Ezekiel Maige, 
aliwaita wadau wote ofisini kwake Dar es Salaam na kuwataka wale 
waliopewa vitalu (vya Wazungu), waelewane kwa lengo la kumaliza 
migogoro.
Baadhi ya wageni hao walikuwa tayari kutoa hadi dola 
milioni moja (Sh zaidi ya bilioni 1.5) ili wazawa wawaachie vitalu 
walivyotaka. Maelekezo ya Waziri Maige yalipingwa na wadau, hatua 
iliyowafanya baadhi ya Wazungu hao, kwa ushirikiano na Watanzania kadhaa
 mawakala wao, watambe kuwa kama wamekataa fedha hizo, watahakikisha 
wanazitumia katika ngazi nyingine ili watwae vitalu walivyovitaka. 
Endapo
 Waziri wa sasa wa Maliasili na Utalii atabariki mapendekezo ya Kamati 
ya Ugawaji Vitalu, atakuwa amekamilisha majigambo ya matajiri hao wa 
kigeni.
Uchunguzi wa MTANZANIA, umebaini baadhi ya kampuni 
zilizopewa vitalu hivyo ni za raia wa kigeni ambazo wakati wa uombaji 
zilijitanabahisha wazi kuwa ni za kigeni, lakini sasa zimebadili na 
kujitambulisha kuwa ni za Kitanzania. Mchezo huo umefanywa ili ziweze 
kupata vitalu na kukamilisha masharti ya kisheria yanayotaka asilimia 85
 ya kampuni zinazopata vitalu, ama ziwe za Kitanzania, au wageni wawemo,
 lakini wakiwa na hisa chache.
Kampuni za wazalendo 
zimependekezwa kunyang’anywa vitalu ilhali ikiwa imesalia miezi mitatu 
tu zikabidhiwe umiliki wa miaka mitano. Endapo mpango huo wa kifisadi 
utatekelezwa, Serikali itaingia matatani kutokana na ukweli kwamba 
kampuni nyingi za Kitanzania zenye sifa zote kisheria zimeshapewa barua 
na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa ajili ya shughuli za uwindaji wa 
kitalii.
Jaji Ihema, alipopigiwa simu jana kuzungumzia tuhuma 
hizo, alikataa kuingia kwenye undani wa suala hilo, kwa maelezo kwamba 
msemaji ni Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Profesa Alexander 
Songorwa. Mkurugenzi huyo naye hakupatikana kupitia simu yake ya 
mkononi.
Mmoja wa wajumbe wa Kamati hiyo, akizungumza kwa 
masikitiko, alisema baadhi ya Watanzania wenye sifa wamenyang’anywa 
vitalu na kupewa Wazungu ambao tangu awali hawakutaka kabisa vitalu 
hivyo wapewe Watanzania. Maeneo manono yenye wanyamapori na yanayopendwa
 na wawindaji wengi, yakiwamo ya Maswa, yote sasa yanamilikiwa na 
kampuni za kigeni, zinazopata nguvu kutoka kwa baadhi ya mawakala wao 
Watanzania.
Habari za uhakika zinaonyesha kuwa mmoja wa 
Watanzania ambaye ni mwanasheria, amehakikisha mpango wake wa muda mrefu
 wa kujitwalia vitalu kutoka kwa Watanzania wenzake wenye uwezo, 
unafanikiwa. Kuna habari kwamba mpango huo umewezekana kutokana na nguvu
 za kifedha na kimamlaka kutoka kwa mmoja wa watoto wa viongozi 
waandamizi kabisa hapa nchini.
Kamati ya Ushauri wa Ugawaji 
Vitalu vya Uwindaji wa Kitalii, pamoja na kutuhumiwa kukumbwa na rushwa,
 imeendelea kuwapo, licha ya wito kutoka kwa wabunge na watu maarufu, 
akiwamo aliyekuwa Mbunge wa Kwela, Dk. Chrisant Mzindakaya.
Chanzo
 cha habari kimesema kwamba ugawaji vitalu uliofanywa wiki iliyopita 
uligubikwa na harufu ya rushwa, kutokana na ukweli kwamba Kamati hiyo 
inatambua wazi kuwa muda si mrefu itavunjwa.
“Walichoamua 
kukifanya baadhi ya wenzetu ni kuhakikisha kuwa wanapata pesa kutoka kwa
 wadau wa vitalu kwa sababu muda wao wa kuwa kwenye Kamati unahesabika,”
 kimesema chanzo chetu.
Chanzo hicho kimesema endapo mapendekezo 
hayo yatatekelezwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis 
Kaghasheki, ni wazi kwamba atakuwa amebariki rushwa na uonevu unaofanywa
 na baadhi ya Watanzania kwa lengo la kuwapendelea Wazungu. 
Kamati
 iliyovunjwa na Balozi Kagasheki, ilikuwa ikiongozwa na Bakari Mbano, 
ambaye amepata kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori mwaka 1995-1998.
Kamati
 hiyo, pamoja na Mbano na Jaji Ihema, inaundwa na Dk. Simon Mduma 
(Mkurugenzi Mkuu TAWIRI), Edward Msyani (kwa niaba Mkuu wa Chuo cha 
MWEKA) na Saidi Nzori (Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali).
Wengine
 ni Allan Kijazi (Mkurugenzi Mkuu TANAPA), Obeid Mbangwa (Mkurugenzi wa 
Idara ya Wanyamapori –ambaye alifukuzwa kazi hivi karibuni), Mbunge wa 
Viti Maalumu Mary Mwanjelwa (CCM), Profesa Leticia Rutashobya (Mhadhiri 
Mwandamizi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam), Daniel Nsanzugwanko (Naibu 
Waziri wa Kazi wa zamani), na Beno Malisa ambaye alikuwa Kaimu 
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM).
 
Wakati wa ugawaji vitalu uliofanywa awali, mgawanyiko mkubwa uliibuka 
ndani ya Kamati kutokana na kila upande kuvutia kwake. Hatua hiyo 
ilitafsiriwa kuwa ilitokana na baadhi ya wajumbe kuhongwa na wenye 
kampuni za uwindaji wa kitalii.
Mei, mwaka huu, aliyekuwa Mbunge 
wa Kwela, Dk. Chrisant Mzindakaya, alizungumza na waandishi wa habari na
 kuishutumu Kamati ya Ushauri wa Ugawaji Vitalu, akisema ilikuwa 
imepoteza maana na akamshauri Waziri mpya wa Maliasili na Utalii, Balozi
 Kagasheki, aivunje haraka.
Alisema, “Baadhi ya wajumbe wa Kamati
 ya Bunge na ile ya Kumshauri Waziri kuhusu Ugawaji wa Vitalu 
walikwishatumbukia katika mtego na kutoa ahadi kwa kampuni hizo kuwa 
watalitumia Bunge kugawa vitalu upya na kwamba watasaidia idadi ya 
kampuni hizo kupanda mpaka asilimia 30 ya uwiano (kutoka asilimia 85 kwa
 wazawa dhidi ya asilimia 15 kwa wageni).
“Iliandikwa katika 
gazeti kwamba huko Dodoma baadhi ya wabunge walikarimiwa kwa njia ya 
semina na mwanasheria anayetumikia baadhi ya kampuni za kigeni. Wabunge 
hao, kwa mujibu wa taarifa hizo, wanadaiwa walipewa posho nono ya semina
 hiyo.
 
No comments:
Post a Comment